Home » » Mahakamani kwa kukutwa na CD za kigaidi, mafunzo ya kijeshi

Mahakamani kwa kukutwa na CD za kigaidi, mafunzo ya kijeshi

MWANAUME mmoja amefikishwa katika mahakama ya mkoa wa Mara, kwa tuhuma ya kukamatwa na CD zenye machapisho ya kigaidi, ambazo zina mafunzo ya kijeshi na zinazochochea vurugu.

Aliyefikishwa katika mahakama hiyo, ametambuliwa kwa jina la Ramadhan Twaha (36) mkazi wa mtaa wa Kirumba jijini Mwanza.
Mwendesha mashitaka wa serikali Bw. Jonas Kaijage, amemsomea mashitaka manne mshitakiwa huyo, mbele ya hakimu mkazi, mfawidhi, mwandamizi wa mkoa wa Mara, Bw. Faisal Kahamba.

Bw. Kaijage amesema kuwa mshitakiwa huyo anatuhumiwa kutenda makosa hayo septemba 27 mwaka huu, katika  msikiti wa Ibadhi ulioko mjini Bunda.

Amesema kuwa mshitakiwa huyo anashitakiwa kusambaza CD zenye machapisho  ya uchochezi, kuuza na kushawishi watu kununua CD zenye picha na maelezo yasioruhusiwa kisheria, pamoja na machapisho na picha zenye mwelekeo wa kigaidi na mafunzo ya kijeshi kinyume cha sheria.

Mtuhumiwa huyo amekana mashitaka yote manne na kupelekwa mahabusu hadi tarehe 21 mwezi huu, kesi yake itakapotajwa tena mahakamani hapo.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa