Home » » Wananchi waomba JWTZ kusaka wavuvi haramu

Wananchi waomba JWTZ kusaka wavuvi haramu

WANANCHI katika wilaya ya Bunda, mkoani Mara, wameiomba serikali kutumia jeshi la wananchi wa Tanzania (JWTZ) katika kukabiliana na uvuvi haramu hasa wa kutumia sumu katika ziwa Victoria, kwa madai kuwa maafisa uvuvi pamoja polisi wameshindwa kuwadhibiti wavuvi hao.

Wananchi hao wameyasema hayo kwenye mkutano wa ndani wa maendeleo uliokuwa umeandaliwa na mkuu wa wilaya ya Bunda, aliyewakilishwa na kaimu Afisa Tarafa ya Kenkombyo, Bw. Abiud Peter Jandwa, na kufanyika katika shule ya msingi Kasahunga.

Wamesema kuwa uvuvi haramu wa kutumia sumu, ambayo sehemu kubwa ni dawa ya kuhifadhia maiti ya binadamu ili isiharibike, umeshamiri sana katika Tarafa za Nansimio na Kenkombyo,  hali ambayo inahatarisha afya za binadamu pamoja na viumbe hai vingine vya majini.

Wameongeza kuwa kutokana na wavuvi hao kuwa na mbinuu nyingi ikiwemo kuvua wakiwa wana silaha mbalimbali zikiwemo za jadi, sasa ni vema jeshi la wananchi ilikaingilia kati na kuwasaka wavuvi hao, kwani inaonekana maafisa uvuvi pamoja na polisi wameshindwa kukomesha hali hiyo.

Aidha, wamesema kuwa pamoja na kuwa mstari wa mbele katika kukabiliana na wavuvi hao, lakini wanakatishwa tamaa na vyombo vya serikali, wakiwatuhumu moja kwa moja polisi kwamba wamekuwa wakiwaachia huru wavuvi hao hasa katika mazingira ya kutatanisha.

Wameongeza kuwa hivi karibuni wananchi wa kijiji cha Buzimbwe pamoja na wanajeshi wa JKT, walipambana na wavuvi hao waliokuwa na pinde na mawe na kufanikiwa kuwakamata watatu, huku wawili wakijitosa majini, ambapo mmoja alikufa maji.

Wamesema kuwa cha ajabu wavuvi watatu waliokamatwa na kupelekwa polisi inadaiwa wameachiwa huru, ingawa walikuwa na vielelezo vyao, ikiwemo sumu pamoja na samaki ambao tayari walikuwa wameshavuliwa.

Wamefafanua kuwa hiyo ni mara ya pili kwa  wavuvi  hao kukamatwa, ambapo kesi nyingine ya kwanza na yenyewe walidhaminiwa katika mazingira ya mashaka.

Kamanda wa polisi mkoani mara, kamishina msaisdizi wa polisi, Bw. Ferdinand Mtui, amesema kuwa atafuatilia suala hilo kwa ukaribu zaidi, ili kupata ukweli wake.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa