Home » » Walimu watuhumiwa kufanya mapenzi na wanafunzi wao

Walimu watuhumiwa kufanya mapenzi na wanafunzi wao

BAADHI ya walimu shule za sekondari katika wilaya ya Bunda, mkoani Mara, wametuhumiwa kuwageuza wanafunzi wa kike kuwa wake zao  kwa kufanya nao mapenzi, hali ambayo imekuwa kero kubwa kwa wazazi na walezi wa watoto hao.

Hayo yameelezwa juzi na kaimu afisa tarafa ya Kenkombyo, Bw. Abiud Peter Jandwa, kwenye kikao kilichoshirikisha wadau mbalimbali wa maendeleo wa tarafa hiyo, na kufanyika katika shule ya msingi Kasahunga.

Bw. Jandwa aliyekuwa anamwakilisha mkuu wa wilaya ya Bunda, Bw. Joshua Mirumbe, amesema kuwa amekuwa akipokea malalamiko mara kwa mara, kutoka kwa wazazi na walezi juu ya kuwepo kwa hali hiyo.

Amesema kuwa wazazi na walezi hao wamekuwa wazkidai kuwa kuna baadhi ya walimu wamegeuza watoto wa kike kuwa wake zao, hali ambayo imekuwa ikisababisha wanafunzi hao kutokufanya vizuri katika masomo yao.

Kufuatia hali hiyo Bw. Jandwa amewaonya walimu wanaofanya mchezo huo mchafu wa kufanya mapenzi na wanafunzi wao, kwani atakayebainika ikiwa ni pamoja na kupatikana ushahidi wa kutosha atachukuliwa hatua kali za kinidhamu na za  kisheria.
Aidha, amewataka wazazi na walezi kufuatilia mienendo ya wanafunzi wao, ikiwa ni pamoja na kuwaonya kutokujiingiza kwenye vishawishi ambavyo kwa namna moja ama nyingine wanaweza kukatisha masomo yao kwa kupata ujauzito.


0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa