Home » » "RASAMU HII ITAFUNGA WENGI'

"RASAMU HII ITAFUNGA WENGI'

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Mwenyekiti wa Vijana Taifa wa Chadema, John Heche
“Kwa rasimu hii ilivyo, kama ikipita na kuwa Katiba, nina hakika viongozi wengi waliotumia vibaya madaraka yao wakati wa uongozi wao na walioko madarakani, wataishia gerezani na itakuwa mwanzo wa mabadiliko ya taifa hili.
Tanzania licha ya kuwa na kila aina ya rasilimali, wananchi wake wameendelea kusota kwa kukosa huduma muhimu za afya, maji, elimu na miundombinu ya barabara ambayo imeendelea kuwa mibovu.
Lakini rasimu hii itawafuta machozi Watanzania na kuanza ukurasa mpya wa maisha yenye matumaini.”
Hayo ni maneno ya Mwenyekiti wa Vijana Taifa wa Chadema, John Heche anapofungua mdomo wake kuzungumza na mwandishi wa makala haya.
Anasema, aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Mstaafu Joseph Warioba, amesikia kilio cha Watanzania na kuandaa Rasimu ya Katiba itakayowabana viongozi waliokuwa wakitumia nafasi zao vibaya, huku wakiwaacha wananchi wanahangaika na ugumu wa maisha.
Heche anaendelea kueleza kuwa Jaji Warioba bila ya kujali kwamba amekuwa kiongozi ndani ya Serikali ya CCM kwa kipindi kirefu, akatanguliza uzalendo kulingana na maoni na mapendekezo waliyoyatoa Watanzania wakati wa kuiandaa rasimu hiyo. “Tume ya Katiba chini ya Jaji Warioba ilifanya kazi ngumu, kubwa na ambayo haikutegemewa na Watanzania,” anasema Heche na kuongeza;
“Kwa kipindi kifupi walichopewa wamekuja na rasimu inayoitetemesha CCM kila wanapoisoma, huku wasijue wanaichakachuaje ili isipite.”
Heche anabainisha kuwa ukiisoma rasimu hiyo, utagundua kuwa imeegemea upande wa wananchi, jambo ambalo ni jema, lakini CCM wanafanya kila njia kuipindisha, jambo ambalo wao hawatakubali kuona likitokea.
“Kama kuna kitu ambacho Watanzania wanatakiwa kukipigania kwa nguvu zote, ni rasimu hii, ambayo wao wameipendekeza na kutokufanya hivyo watakuja kujuta wenyewe,” anasema.
Tunu za Taifa
Heche anasema kwa kuona kuwa taifa limepoteza mwelekeo, Jaji Warioba ameamua kuweka tunu za taifa ambazo ni Utu, Uzalendo, Uadilifu, Uwazi, Uwajibikaji, Umoja na Lugha ya taifa ili viweze kuliongoza taifa.
Anasema Serikali imekuwa ikifanya mambo yake ambayo yanahusu maslahi ya Watanzania kwa kificho na kuliweka taifa njia panda kutokana na uzembe na ubinafasi wao. “Jaji Warioba amesema kila kitu kitafanywa kwa uwazi, kama ni kusaini mikataba basi iwe ni wazi ili wananchi wajue mikataba hiyo inayosainiwa inawanufaisha akina nani.
Rasilimali ambazo Mungu amelijalia taifa hili kama gesi, madini, dhahabu, makaa ya mawe na mengine mengi, lakini wananchi bado wanalia na ugumu wa maisha! Yote haya yamesababishwa na kusaini mikataba kwa uficho.
Alifafanua kuwa viongozi wengi wamekuwa si waadilifu, lakini Rasimu hii imezuia matumizi mabaya ya madaraka kwa kujineemesha na kuacha kuwatumikia wananchi.
“Hivi sasa mtu akipata kazi basi maisha yake yanabadilika ghafla ndani ya muda mfupi, lakini kwa rasimu hii hakuna mtu au kiongozi atakayefuja mali ya umma ovyo, kwani atajiweka kitanzini mwenyewe,” anasema Heche.
Mustakabali wa CCM
Mwenyekiti huyo anasema Mchakato wa Mabadiliko ya Katiba, utahitimishwa na wananchi na wala si chama tawala (CCM).
Anasema hakuna nchi yoyote duniani iliyowahi kuandika Katiba kwa kushirikisha kundi moja.
“Mwisho wa CCM ndiyo umefika, wakiipinga rasimu hii najua wananchi hawatakubali kuona mapendekezo yao yanatupwa nje hivyo nao wataitupa katika uchaguzi ujao na hapo ndipo ukurasa mpya utakuwa umeanza,” anasema Heche na kuongeza:
“CCM imekuwa haina amani tangu Rasimu hiyo ilipozinduliwa Desemba 30 mwaka jana kutokana na Rasimu nzima kuegemea upande wa wananchi wakati wakijitazama wenyewe wanaona maji yako shingoni.”
Heche anasema: “CCM wamekuwa wakisema Jaji Warioba ni msaliti kwa kuandaa rasimu ambayo wao hawakupendezwa nayo. Sasa mimi nawaomba wajitokeze kwa wananchi wawaeleze ni kipengele gani kilichomo ndani ya rasimu hiyo kinachowabana wananchi na kitarudisha nyuma maendeleo yao pindi wakiipitisha kuwa Katiba.”
Anasisitiza kuwa rasimu hii ni nzuri na inafaa kupitishwa bila vikwazo.
Anafafanua kuwa: “Rasimu inasema ukifikisha miaka 60 hata kama ni mkulima, mchoma mahindi, fundi nguo, baiskeli utatakiwa kulipwa pensheni ya uzeeni sambamba na wafanyakazi wengine na CCM wanapinga jambo hili.”
Chanzo:Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa