Home » » SERIKALI BUNDA YAKEMEA UKABILA

SERIKALI BUNDA YAKEMEA UKABILA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
MKUU wa Wilaya ya Bunda, Joshua Mirumbe, amekemea ubaguzi wa kikabila kati ya Wajaluo na Wajita, ulioanza kujitokeza katika Kijiji cha Karukekere, kilichoko wilayani Bunda, mkoani Mara.
Mirumbe, alitoa onyo hilo juzi kwenye mkutano wa hadhara wakati akihutubia wananchi kijijini hapo, ambapo alisema atakayethubutu kuleta chokochoko za kikabila atachukuliwa hatua kali za kisheria.
Alibainisha kuwa dalili za ubaguzi kati ya Wajaluo na Wajita zimeanza kujitokeza katika kijiji hicho na serikali haiwezi kuzivumilia kwa sababu zinahatarisha amani.
“Sitaki kusikia tena hali ya ukabila katika kijiji hiki, na wilayani kwangu kwa ujumla, kama ni suala la uhamiaji haramu linashughulikiwa na ofisi ya Uhamiaji kuliko baadhi yenu kujifanya ndio wenye jukumu hilo,” alisema.
Mirumbe, alimuagiza Mwenyekiti wa kijiji hicho, Jogoro Amoni na Diwani wa Kata ya Namhura, Okore Manase, washirikiane na wananchi badala ya kuweka mbele itikadi za vyama vya siasa.
“Ninawataka nyinyi viongozi mshirikiane pamoja ili wananchi waweze kufanya kazi za kujiletea maendeleo na si kila wakati kushikilia misimamo ya vyama na kulumbana na mnaingiza ukabila eti wahamiaji haramu… nchi haiwezi kuendeshwa kwa mtindo huo hata kidogo,” alisema.
Katika kikao hicho, diwani na mwenyekiti huyo waliwaomba radhi wananchi kuwa wao wamechangia kuwepo kwa hali ya kutoelewana kijijini hapo.
Siku za hivi karibuni ulitokea ugomvi uliosababisha vijana watatu wa kabila la Wajaluo kujeruhiwa na kulazwa hospitalini baada ya kutokea ugomvi kwa makabila hayo mawili.
Chanzo:Tanzania Daima 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa