Home » » WAZIRI CHIKAFWE,IGP MANGU NA CHANGAMOTO ZA USALAMA TARIME

WAZIRI CHIKAFWE,IGP MANGU NA CHANGAMOTO ZA USALAMA TARIME

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Viongozi mbalimbali  wakimsikiliza Waziri wa Mambo ya Ndani, Mathias Chikawe wakati wa ziara yake Nyamongo

Kumekuwapo malalamiko mengi baina ya wananchi, wenye migodi wa eneo la Nyamongo wilayani Tarime na askari wa Jeshi la Polisi katika mkoani Mara.
Mzozo huo umesababisha kutoweka kwa amani , usalama na tuhuma nyingi za mauaji zinazoelekezwa kwa polisi.
Polisi wa kituo cha Nyamongo, hasa wale wanaolinda mgodi wa dhahabu wa Africa Barrick Gold Mine (ABG) wanalalamikiwa kuwanyanyasa wananchi kwa kuwapiga na kuwajeruhu kwa risasi na wengine kuuawa.
Pia, askari walioajiriwa na mgodi ambao wanajulikana kwa jina la Mobile, nao wanatuhumiwa kuhusika katika mauaji ya wananchi wanaodaiwa kuingia mgodini kwa nia ya kuokota mawe ya dhahabu.
Mbali na tuhuma hizo kuelekezwa kwa polisi na mgodi, Serikali nayo inalalamikiwa kwa kushindwa kutatua kero za wananchi wake badala yake hutumia nguvu nyingi kupambana na wananchi na kusababisha uvunjifu wa amani.
Waziri wa Mambo ya Ndani ambaye pia ni mbunge wa Nachingwea, Mathias Chikawe akiongozana na waziri kivuli wa Mambo ya Ndani, Vicent Nyerere ambaye pia ni mbunge wa Musoma Mjini (Chadema) na mkuu wa Jeshi la Polisi, IGP Ernest Mangu walifika Tarime kujua sababu za kutokuwapo kwa usalama katika eneo la Nyamongo.
“Nimekuja Nyamongo kujifunza kwa sababu nimekuwa nikisikia kuwa hali ya ulinzi na usalama hakuna; mara watu wanauawa na polisi; na mgodi nao unadai wananchi wanauvamia. Naombeni nipate taarifa nijue nini tatizo,” alisema Waziri Chikawe.
Kaimu Meneja wa mgodi ambaye pia ni meneja machimbo, Jimmy Ijumba anasema kuwa uhalifu na uvamizi wa mgodi ni changamoto kubwa inayosababisha ugumu katika utawala wa kisheria, na wananchi wamekuwa wakiiba dhahabu na kuharibu mali na hivyo mgodi kuingia hasara. alisema wananchi huvamia wakiwa na silaha za jadi.
“Wavamizi huingia mgodi hasa kipindi ambacho shule zimefungwa kwa kuwa kunakuwa na idadi kubwa ya watu. Zaidi ya watu 100 huvamia. Uvamizi ukizidi shughuli za uzalishaji zinasimama. Mgodi ukisimama kwa saa moja bila kufanya kazi tunapoteza Dola 24,000 sawa na karibu Sh30 milioni,” anasema.
Anaeleza kuwa kutokuwapo kwa hali ya usalama kumesababisha wafanyakazi wa mgodi kutochangia mapato ya biashara za wananchi kwa kuhofia usalama wa maisha yao. Wapo baadhi ya wafanyakazi wameshatekwa, kupigwa na kunyang’anywa mali.
Kwa upande wa miradi, Ijumba anasema mgodi umekuwa ukisaidia shughuli kama za ukarabati wa shule na kituo cha afya Nyamongo na maji lakini miundombinu huharibiwa na wananchi na kusababisha mgodi kuingia hasara kubwa. Alisema jamii inapaswa kubadilika kwa kuwa kuna kampuni nyingi zilizotangulia lakini haikutekeleza miradi ya wananchi tofauti na ilivyo sasa kwa ABG.
Aeleza sababu za vifo
Ijumba alikanusha taarifa kuwa watu walio wengi hufia mgodini, lakini akabainisha kuwa wananchi wenyewe huchomana visu wakati wakigombania mawe ya dhahabu.
“Huchomana visu na kusukumana kwenye shimo na wakati mwingine huangukia kwenye shimo lenye urefu wa mita 200-300 na wasipoelewana hupigana hadi kuuana,” anasema.
Kuhusu Fidia
Meneja huyo anasema kuwa kumekuwa na tatizo la watu kutegesha nyumba wakizijenga kwa lengo la kufanyiwa tathimini ili mgodi uwalipe fedha na wanapolipwa huzikataa kwa madai kuwa ni kidogo ambapo hadi sasa kuna Sh5 bilioni za malipo ya fidia hazijachukuliwa.
Waziri Chikawe na timu nzima yake wakazungukia maeneo yote ya mgodi kwenye maeneo yanayodaiwa wananchi huruka ukuta na kuingia ndani kuiba dhahabu.
Pia, akaonyeshwa nyumba zilizojengwa kwa kutegeshwa kwenye maeneo jirani na mgodi ambako awali hapakuwa na nyumba. Alieleza kuwa nyumba hizo zilijengwa baada ya kupata taarifa kuwa kuna maeneo yatafanyiwa thamini kupisha shughuli za mgodi.
Waziri Chikawe alikagua baadhi ya miradi iliyotekelezwa na mgodi, ikiwa ni pamoja na ukarabati na ujenzi wa Shule ya Sekondari ya Ingwe, kituo cha afya Nyamongo na ujenzi wa Shule ya Msingi Nyangoto na Matare.
Mkutano wa waziri viongozi wa vijiji
Waziri Chikawe alikutana na madiwani na viongozi wa serikali za vijiji saba vinavyozunguka mgodi ili kupata malalamiko yao ikiwa ni pamoja na kujua tatizo la usalama, kikao kilichofanyika Shule ya Sekondari ya Ingwe.
Mwenyekiti wa Kijiji cha Kewanja kwa tiketi ya Chadema, Tanzania Omtima aliilaumu Serikali kwa kumkaribisha mwekezaji aliyekuta maeneo yakimilikiwa na kuchimbwa na wananchi kisha kuyachukua bila kuangalia namna gani itawawezesha wananchi baada ya machimbo yao kuchukuliwa na mwekezaji.
“Chanzo cha kukosekana kwa amani Nyamongo ni Serikali. Wawekezaji walipewa maeneo makubwa. Asilimia 80 ya Wanyamongo tangu zamani walikuwa wanategemea dhahabu sasa hawana mahali pengine pa kupata riziki, hali hiyo imesababisha mwananchi kutojua umuhimu wa mwekezaji ukizingatia mgodi unachelewa kutekeleza miradi kwa mujibu wa makubaliano,” anasema Omtima.
Diwani wa viti maalum, Filomena Tontora (Chadema) anasema: ”Hii Kampuni imeleta migogoro imetuvunjia amani. Enzi za mwekezaji wa kwanza (kampuni ya Afrika Mashariki Gold Mine, AMGM), hapakuwa na matukio kama haya. Wazungu walikuwa wanazunguka kila mitaa wanakula chakula kwenye hoteli zetu.”
Anaongeza kuwa wazungu wale walijiita kwa majina ya Kikurya kama, Bhoke, Chacha, Ghati, Marwa na mengineyo.
Anaeleza kuwa Jeffer alipokuwa akiona mtoto anachimba dhahabu au siku za shule akikutana na mtoto, anamuuliza ‘mbona hujaenda shule?’ Mtoto anajieleza. Alisomesha watoto, akiwamo Ghati Juma ambaye ni mwanasheria wa mgodi, ila tangu Barrick Iwekeze ni majanga kwani kuna mauaji kila siku mgodini,” anasema Tontora.
Diwani wa Kata ya Kemambo, Wilson Mangure (Chadema) anawatuhumu polisi wa Nyamongo kwa ukamataji holela, hata kwa watu wasio na hatia na kuwabambikia kesi za uvamizi mgodini na wizi wa kutumia silaha.
Diwani wa viti maalumu wa Nyamongo (CCM), Mwajuma Issa anasema kuwa kazi ya polisi ni kulinda raia na mali zake, lakini polisi wa Nyamongo wanajiamulia kwenda kukamata watu, wanafukuza watu nyumbani kwao.
“Wanapekua kwenye magodoro wakikuta simu au pesa wanabeba wanaondoka navyo na ukikamatwa, hupelekwi kutuoni wanakuomba pesa Sh100,000 hadi 200,000. Ukikataa ndiyo wanakupeleka kituoni wanakubambikia kesi za uongo kwa kisingizio kuwa Wakurya ni wakorofi,” anasema Mwajuma.
Mwenyekiti wa Kijiji cha Nyangoto, Elisha Nyamuhanga (CCM) anasema: “Utawala bora haupo Tarime. Viongozi wa ngazi za juu wakija Nyamongo viongozi wa serikali za vijiji hatujulishwi hata ujio wako tumekurupushwa. Mnaonyeshwa na watu wa mgodi miradi iliyo ndani ya kijiji hata mwenyekiti wa halmashauri hakushirikishwa,” alisema.
Diwani wa viti maalumu, Loyce Chacha anasema Serikali ndiyo inawachonganisha wananchi na mgodi kwa kuwa tayari watu walishafanyiwa tathmini na kikosi kazi kutoka Serikalini. Kwa kushirikiana na mgodi, walifanya tathmini ili watu wahame maeneo kupisha shughuli za mgodi, lakini ni mwaka sasa watu hawajalipwa fedha licha ya kuwa walisimamishwa kuendesha shughuli kwenye maeneo hayo.
Kauli ya majumuisho ya Chikawe
Waziri Chikawe aliwajibu viongozi hao kuwa malalamiko hayo yamemfanya ajifunze mengi. “Uzuri tumeingia viongozi wapya, mimi na IGP, ambao tunataka usalama uimarike, polisi wafanye kazi kwa maadili. Tulishawaambia kuwa polisi atakayeenda kinyume atawajibishwa msiogope nipigieni simu namba zangu ni 0685777222 nitachunguza nikithibitisha anawajibishwa,” alisema Chikawe.
Alisema baada ya kukamilisha ziara yake ya siku moja wilayani hapo, amegundua kuna tatizo la uhusiano usioridhisha baina ya mgodi wa North Mara na wananchi wa vijiji saba vinavyozunguka mgodi na kusababisha kutokuwepo kwa usalama.
Chikawe anaeleza kuwa kutokuwepo kwa uhusiano mzuri kumechangia kuwapo kwa migogoro kati ya mwekezaji na wananchi, hivyo akauomba mgodi kujenga uhusiano ikiwa ni pamoja na kusaidia katika miradi mbalimbali inayogusa jamii kama afya na maji
Chanzo:Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa