Home » » WAZAZI WANACHANGIA WATOTO KUFELI

WAZAZI WANACHANGIA WATOTO KUFELI

 http://www.mwananchi.co.tz/image/view/-/2573302/highRes/910658/-/maxw/600/-/rvdj6sz/-/mwalimu_darasani.jpg
Hata hivyo, jitihada hizi hivi sasa zinaonekana kuzorota na dalili zinaonekana katika ubora unaotia shaka wa elimu inayotolewa kwenye taasisi husika.
Matokeo ya mitihani ya kitaifa katika miaka ya hivi karibuni yanashadadia ukweli wa hali mbaya ya elimu ilivyo shuleni.
Mfano mzuri wa matokeo hayo ni yale ya kidato cha nne ya mwaka 2012, ambayo yameacha historia ya kusikitisha katika sekta ya elimu kutokana na idadi kubwa ya watahiniwa kufanya vibaya katika mitihani yao.
Katika matokeo hayo, asilimia 60 ya watahiniwa walipata daraja sifuri. Wapo watahiniwa ambao hawakuamini matokeo hayo kiasi cha wengine kufikia hatua ya kujitoa uhai. Lakini wapo waliokata rufaa ili warudie mitihani upya.
Kwa kuwa matokeo hayo yalizusha mjadala mkubwa wa kitaifa, Serikali ililazimika kuunda tume maalumu kuchunguza sababu za matokeo hayo kuwa mabaya.
Kimsingi, watu wengi wanaamini kuwa miongoni mwa sababu kubwa zilizochangia matokeo hayo ni migomo ya walimu, mazingira duni ya kufundishia, kukosekana kwa mtalaa na ukosefu wa walimu wenye sifa shuleni.
Hata hivyo, Profesa Kitila Mkumbo wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam anasema hoja ya mtalaa inayopigiwa kelele kila kukicha, siyo sababu ya msingi ya kufeli kwa wanafunzi.
Ni wazi kuwa masuala mengine yanayochangia ufaulu mdogo katika mitihani ni wazazi kutowajibika kusimamia maendeleo ya taaluma ya watoto wao.
Kwa mtazamo wake, mchango wa wazazi katika ufaulu wa mwanafunzi unachukua asilimia kubwa kuliko muda anaoutumia akiwa shuleni.
Wadau wa elimu wanasema hadi sasa ufuatiliaji wa wazazi ni asilimia mbili tu nchini ukilinganisha na mataifa mengine.
Jukumu la mzazi ni kuhakikisha anafahamu mwenendo wa tabia za mwanaye shuleni, lakini sasa kazi hiyo wameachiwa walimu na watendaji wengine.

Sababu kubwa ya wazazi kutokuwa karibu na watoto wao zinaelezwa kuwa ni pamoja na mazingira ya nyumbani.
Jambo la kujiuliza mtoto anaporudi kutoka shuleni kila siku anakutana na kitu gani? Kama baba ni muuza nyanya basi ni sahihi akutane na matenga ya nyanya kama ilivyo kwa mwalimu atavyokutana na vitabu?
Wazazi wengi hawana muda wa kukaa na watoto wao kujadili masuala ya elimu, badala yake wamekuwa mstari wa mbele kulalamika mambo yanapoharibika kama ilivyotokea katika matokeo ya mitihani hiyo.
Haiwezekani mwanafunzi amalize mwaka mzima wa masomo bila ya mzazi wake kumuulizia kuhusu maendeleo yake. Huku ni kutowajibika kulikozidi.
Mwanafunzi Edmond Elia wa Shule ya Msingi Mburahati, anasema anaweza kukaa kipindi kirefu bila ya kuhojiwa au kukaguliwa maendeleo yake shuleni.
Anasema kila anaporudi nyumbani na wenzake, hutumia muda wake mwingi kwenda katika mazoezi ya mpira wa mguu.
“Sijawahi kuulizwa maendeleo yangu ya shuleni tangu niingie darasa la saba, ni mara chache hutokea mzee wangu kukagua madaftari yangu,” anasema.
Baba mzazi wa Edmond ni mfanyabiashara wa maziwa, hivyo muda mwingi anamtumia mwanawe kumsaidia katika biashara zake anapotoka shuleni badala ya kumhimiza kujisomea akiwa nyumbani.
Huyu ni mmoja kati ya maelfu ya wanafunzi ambao wazazi wao hawana mpango nao katika maendeleo.
Watanzania tubadilike kwa kuchukua hatua za kufuatilia kwa ukaribu mienendo ya watoto wetu badala ya kuitupia lawama Serikali hasa mambo yanapoonekana kwenda mrama katika sekta ya elimu
Chanzo:Mwananchi
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa