Home » » DC:MARUFUKU KUSAFIRISHA MIFUGO USIKU.

DC:MARUFUKU KUSAFIRISHA MIFUGO USIKU.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Imeandikwa na Samson Chacha, Tarime
Mkuu wa Mkoa wa Mara, Magesa Mulongo.
MKUU wa Wilaya Tarime mkoani Mara, Glorius Luoga amepiga marufuku kusafirisha mifugo usiku wilayani humo, ikiwa ni hatua ya kudhibiti wimbi la wizi wa mifugo. Aidha, ametangaza vita na wakulima, wasafirishaji, wauzaji na watumiaji wa bangi kwani matumizi yake, yamechangia kukithiri uhalifu wilayani humo.
Luoga alisema hayo wakati wa Kongamano lililoandaliwa na kikao cha Mkuu wa Mkoa wa Mara, Magesa Mulongo mjini hapa. Kongamano hilo lilihudhuriwa na viongozi wa serikali, wa kidini na kimila, Polisi wilaya ya Rorya, wenyeviti na wakurugenzi wa halmashauri na watumishi wa kawaida.
Mkuu huyo wa Wilaya alisema kutokana na matukio mengi ya wizi wa mifugo yanayoibuka kila siku, amepiga marufuku usafirishaji wa mifugo nyakati za usiku. Alisema usafirishaji huo, unawachanganya wanaoibiwa mifugo ambayo mingi huibwa usiku.
“Kwa nini mfanyabiashara halali asisafirishe mifugo yake mchana badala yake asafirishe usiku? Hapo kuna jambo la uhalifu ukiwemo wa kukwepa kodi na ushuru halali wa Serikali,” alisema Luoga.
Kuhusu bangi, Luoga alisema uongozi wa Wilaya unatangaza vita na wakulima wa bangi, wasafirishaji na wauzaji wa zao hilo kwani matumizi yake yamewaathiri vijana wengi wenye nguvu kazi na wamejiingiza katika uhalifu.
Alisema mwananchi atakayetoa taarifa za siri za kuwepo na mashamba ya bangi katika eneo fulani na kufanikiwa kukutwa shamba hilo, atapewa zawadi ya Sh 100,000 papo kwa hapo. Aliwataka wananchi wawafichue watu hao.
CHANZO: HABARI LEO.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa