Home » » Wahamao madhehebu ya dini kuvuruga amani waonywa

Wahamao madhehebu ya dini kuvuruga amani waonywa

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Kamanda wa Polisi Tarime/Rorya, Andrew Satta
VIONGOZI wa madhehebu ya dini za Kikristo na Kiislamu zaidi ya 100, wamekutana katika kongamano na kuwaonya baadhi ya watu wanaotumia mgongo wa makanisa na misikiti kuhama madhehebu kwa lengo la kuvuruga amani.
Kongamano hilo lilihudhuriwa na viongozi wa kiserikali wakiwa wanane wa tarafa na wazee mashuhuri wilayani Tarime na Rorya, mkoani Mara, na wamedhamiria kulinda amani ndani ya nyumba za ibada na nchini kwa ujumla.
Kwa nyakati tofauti walidai wenye lengo la kuhatarisha amani ni waumini wanaohamahama madhehebu bila sababu za msingi na kuonya kuhusu tabia hizo. Walisema miongoni mwa watu hao wamo wanasiasa wanaojipenyeza katika madhehebu kwa nia ya kutaka kuwagawa wananchi.
Kongamano hilo lililofanyika katika ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Tarime, liliandaliwa na Kamanda wa Polisi Tarime/Rorya, Andrew Satta na kuhudhuriwa na viongozi hao.
Akizungumza katika kongamano hilo, Satta alisema viongozi wa dini wana umuhimu mkubwa wa kuielimisha jamii katika ibada kwani kumekuwa na wasio waaminifu walioanza kujitokeza na kujipenyeza katika misikiti na makanisa kufanya uhalifu.
“Vitendo vya uhalifu kama vilivyojitokeza katika miji ya Mwanza na Tanga tunavilaani sisi jeshi la Polisi kwa kushirikiana na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya wilaya za Tarime Rorya,” alisema.
Alisema, wanawaomba viongozi wa dini kuwafichua waumini wasio waaminifu wanaojificha katika madhehebu yao kwa nia ya kufanya uhalifu ili wakamatwe na kuwahoji.
Alionya watu wasiwaamini wageni bila kuwa na uhakika nao na shughuli zao na kuwataka watoe taarifa kwa vyombo vya usalama ili hatua zichukuliwe mapema.
Shehe wa Msikiti Mkuu wa Tarime Mjini, Idd Mohamed alisema, “Kuna waumini wengi katika misikiti yetu hapa katika wilaya zetu hizi mbili ambao si raia na wamekuwa wakitoa mahubiri katika misikiti yetu na mengi ya mahubiri yao yanaonekana kupingwa na waumini wenzao”.
Aliwaomba viongozi wa serikali na wa vyombo vya usalama kufuatilia na kuchunguza baadhi ya wageni hao ambao hata wao wanashindwa kuwafukuza kwa kuwa ni kinyume na imani.
Naye Mchungaji John Maguge wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Tarime, alisema hivi karibuni kuwa katika lao wakati wakifungisha ndoa walikuja vijana wawili waliokuwa wamevaa kanzu na kaptula zilizofika kwenye magoti na kofia na kukaa kimya pembezoni mwa kanisa.
“Tuliwahoji na kuwaondoa baada ya kugundua kuwa walitaka kuvuruga kufungwa kwa ndoa hiyo. Tusiwaamini watu tusiowajua wala kuwafahamu wengine ni hatari kwetu tuchukue tahadhari mapema kabla ya matukio ya uhalifu,” alisema mchungaji Maguge.
Askofu John wa Kanisa la FPCT, Tarime alisema viongozi wa dini wanatakiwa kushirikiana na Polisi kwa juhudi zao za kuleta amani kwani kama hakuna amani hata wao katika madhehebu hawataweza kusali wala kuleta maendeleo kwa jamii.
CHANZO GAZETI LA HABARI LEO
 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa