Home » » WANAFUNZI 2 WAFA WAKIANDAA CHAKULA

WANAFUNZI 2 WAFA WAKIANDAA CHAKULA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Imeandikwa na Ahmed Makongo, Bunda
WANAFUNZI wawili wa shule ya msingi Sarawe iliyoko tarafa ya Chamriho halmashauri ya wilaya ya Bunda mkoani Mara, wamekufa na wengine sita kujeruhiwa baada ya kuangukiwa ukuta wa chumba cha darasa wakati wakipembua mahindi kwa ajili ya chakula chao.
Tukio hilo lilitokea juzi majira saa kumi jioni wakati wa saa ya mapumziko katika eneo la shule hiyo. Wanafunzi waliokufa katika tukio hilo ni pamoja na Anastazia Wazilana (8) aliyekufa papo hapo na Amosi Stima Igala (8) aliyekufa wakati akikimbizwa katika hospitali ya rufaa ya Bugando jijini Mwanza kwa ajili ya matibabu zaidi, ambapo wote walikuwa wanasoma darasa la pili shuleni hapo.
Mganga mkuu wa halmashauri ya wilaya ya Bunda ,Dk Nuru Yunge amethibitisha vifo hivyo na kwamba majeruhi walipelekwa kituo cha afya Ikizu na wengine wamehamishiwa katika hospitali ya DDH Bunda.“Pale kituo cha afya Ikizu tulipokea majeruhi saba, na wengine wawili tukawahamishia katika hospitali ya DDH Bunda, kutokana na hali zao kuwa mbaya, lakini kwa taarifa niliyopata majeruhi mmoja amekufa wakati akipelekwa katika hospitali ya rufaa ya Bugando,” alisema.
Ofisa tarafa ya Chamriho Boniphace Maiga, aliwataja wanafunzi waliojeruhiwa kuwa ni pamoja na Happynes Mussa (13) wa darasa la tano, Wambura Nyamrosha (12) wa darasa la nne, Sara Wazilana (14) wa darasa la sita, Emmanuel Mkiriti (8) wa darasa la pili, Mugaya Galinde (8) wa darasa la pili na Pili Juma Matwiga (7) wa darasa la kwanza.
Maiga alisema kuwa chanzo cha ajali hiyo ni ukuta wa darasa hilo kuwa na ufa wa siku nyingi, ambapo uliporomoka na kuwaangukia wakati wakianda mahindi kwa ajili ya chakula cha wanafunzi shuleni hapo, kinachotolewa na shirika la PCI. “Wakati wa mapumziko wanafunzi hao walikuwa nje ya darasa hilo wakipembua mahindi ya PCI na ghafla ukuta huo ulidondoka na ulikuwa na ufa mkubwa siku nyingi. Mwanafunzi mmoja alifia hapo hapo na mwengine amekufa wakati akikimbizwa Bugano baada ya kuwapatia rufaa,” alisema.
Baadhi ya mashuhuda akiwemo katibu wa huduma za jamii katika serikali ya kijiji cha Sarawe, Richard Karangi, walilielezea tukio hilo kuwa ni la kusikitisha, ambapo muuguzi mmoja katika hospitali ya DDH Bunda, alizungumzia hali ya majeruhi mmoja aliyempokea kwamba inaendelea vizuri.
Kamanda wa polisi mkoani Mara, Jafari Mohamed hakupatikana kuzungumzia tukio hilo, lakini polisi wilayani hapa wamethibitisha kuwepo kwa tukio hilo. Wakati huo huo, baadhi ya wananchi waliozungumza na waandishi wa habari walisema kuwa ipo haja ya wakaguzi wa shule kukagua majengo ambayo hayana ubora na kuagiza yasitumiwe na wanafunzi ili kuepusha majanga kama hayo ambayo siyo ya lazima yasitoke tena.
CHANZO HABARI LEO

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa