Home » » 19 wakosa makazi baada ya nyumba zao kubomolewa

19 wakosa makazi baada ya nyumba zao kubomolewa

FAMILIA ya watu 19 wilayani Bunda, mkoani Mara, hawana mahali pa kuishi baada nyumba zao tano kubomolewa kutokana na amri ya mahakama ya baraza la nyumba na ardhi katika wilaya ya Musoma, kwa kile kilichodaiwa kuwa mmiliki wa nyumba hizo alikuwa amevamia ardhi ya mtu mwingine.

Tukio hilo limetokea juzi katika kijiji cha Guta B, wilayani humo, ambapo nyumba hizo ni mali ya Hitinde Chacha, mkazi wa kijiji hicho ambaye ana familia ya watu 19.

Mwenyekiti wa kijiji cha Guta B, Bw. Kisheri Miyange, amethibitisha kuwepo kwa tukio hilo na kwamba kwa sasa wanafamilia hao wakiwemo watoto wadogo wanalala nje.

Bw. Miyange amesema kuwa siku ya tukio dalali mmoja akiwa na askari polisi walifika kijijini hapo na kusema kuwa wanazibomoa nyumba hizo kwa idhini ya baraza la nyumba na ardhi, kwa sababu mmiliki wa nyumba hizo alivamia ardhi ya mwananchi mwingine.

Amesema kuwa walikodi vijana waliowasaidia kubomoa nyumba hizo pamoja na maghara ya kuhifadhia vyakula.

Mmiliki wa nyumba hizo, Bw. Hitinde Chacha amesema kuwa wakati nyumba zake zinabomolewa yeye pamoja na wake zake hawakuwepo bali kulikuwa na watoto wadogo.

Bw. Chacha amesema kuwa baadhi ya vitu vyake vimeporwa na wabomoaji hao zikiwemo fedha tasilimu alizokuwa ameuza ng’ombe wake na kwamba chakula kilichokuwa magharani kimeharibiwa na watu hao.

Aidha, amesema anawasiliana na watu wa haki za binadamu kutoa kilio chake kwani hakutendewa haki.

Mwenyekiti wa baraza la nyumba na ardhi wilayani Musoma hakupatikana kuzungumzia suala hilo, na juhudi za kumtafuta bado zinaendelea.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa