Home » » Mbunge awataka vijana kuunda vikundi

Mbunge awataka vijana kuunda vikundi

na Berensi Alikadi, Musoma
MBUNGE wa Musoma Mjini, Vincent Nyerere (CHADEMA), amewataka vijana katika jimbo hilo kujiunga na kuanzisha vikundi mbalimbali ili iwe rahisi kupewa mikopo itakayowasaidia kujiendeleza kiuchumi.
Nyerere alitoa ushauri huo jana alipozungumza na wajumbe wa mkutano mkuu wa chama hicho Kata ya Kitaji katika mkutano uliofanyika Shule ya Msingi Musoma.
Alisema njia pekee ya vijana kujikwamua katika umaskini ni kuanzisha vikundi na kuvisajili, ili waweze kuomba mikopo kutoka serikalini na kwenye taasisi za kifedha.
Alisema yeye kama mbunge hayuko tayari kugawa pesa kwa kila kijana, kwani si sera ya chama chake, bali atakachofanya ni kuwasaidia vijana namna ya kuandika michanganuo mbalimbali kwa ajili ya kupata mikopo.
“Nataka niwaambie vijana wenzangu, mimi sitaweza kugawa sh 50,000 kwa kila kijana wa jimbo hili, uwezo huo sina, lakini pia si sera ya CHADEMA, bali nawaomba vijana mjiunge katika vikundi na mvisajili ili niweze kuwasaidia namna ya kupata pesa kutoka kwa wafadhili,’’ alisema Nyerere.
Katika hatua nyingine, mbunge huyo aliwataka wanachama wa chama hicho kuachana na maneno ya propaganda zinazoenezwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuwa hajafanya kitu na kwamba wananchi wanaona tofauti iliyopo kati yake na mbunge aliyetangulia.

CHANZO TANZANIA DAIMA 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa