Home » » Bunda waanza kukamua alizeti

Bunda waanza kukamua alizeti

WILAYA ya Bunda, mkoani Mara kupitia shirika lisilo la kiserikali lijulikalo kama MAF, limefunga mashine tatu za kukamulia alizeti katika kata tatu za wilaya hiyo, ikiwa ni sehemu ya mkakati wake wa kupambana na umaskini.
Kata zilizofungwa mashine hizo ni Mugeta na Bunda, zilizoko Tarafa ya Serengeti na Kata ya Kibara iliyopo Tarafa ya Nansimo.
Akizungumza katika uzinduzi wa mashine hizo mwishoni mwa wiki katika Kijiji cha Mugeta, Mwenyekiti Mtendaji wa shirika hilo, Respice Mkama, alisema lengo la mradi wao ni kuwawezesha wakulima wa zao hilo kukamua na kuuza mafuta yao.
Alieleza kuwa mashine hizo aina ya Whriston kutoka China zimegharimu zaidi ya sh milioni 40, zina uwezo wa kukamua tani tano hadi nane kwa siku na kwamba ana imani wakulima wa kata hizo watanufaika na kuondokana na umaskini.
“Katika utafiti wetu tuliofanya tuliona alizeti inasitawi katika maeneo ya kata hizo na ni zao zuri linaloweza kuwaondolea umaskini badala ya kulima pamba pekee,” alisema.
Mkama alisema zao hilo linaweza kukomaa kwa miezi mitatu na kila gunia lina uwezo wa kutoa lita 25 za mafuta, hivyo kuwataka wakulima wa maeneo hayo kuchangamkia fursa hiyo, kwani kuna soko la uhakika.
Ofisa Kilimo wa halmashauri hiyo, Balisimaki Shija, alisema kupitia agizo la mkuu wa wilaya hiyo alilotoa wiki iliyopita ni lazima kila mkulima alime ekari mbili za zao hilo kama zao la biashara licha ya kuwapo zao la pamba.
Alisema halmashauri hiyo itatoa mbegu za ruzuku kwa wakulima, hivyo akawatoa wasiwasi wakulima na kuwataka walime zao hilo kwa wingi.
Mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Joseph Malimbe, ambaye alikuwa mgeni rasmi katika uzinduzi huo alisema alizeti ni zao linaloongeza tija kwa wakulima katika mazao ya biashara.
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa