Mara
NYUMBA 67 zimeezuliwa na nyingine kubomolewa katika
Kijiji cha Mwibagi, wilayani Butiama kufuatia mvua kubwa iliyonyesha juzi.
Akizungumza na Tanzania Daima jana, Ofisa Mtendaji
wa kijiji hicho, Moses Stephano, alisema kuwa mvua hiyo iliyoambatana na upepo
mkali na mawe ilianza kunyesha saa nane mchana hadi saa tisa.
Alisema kuwa mbali na nyumba hizo pia Kanisa
Katoliki lililopo kijijini hapo pamoja na stoo ya kikundi cha kuzaliwa mbegu za
mazao nazo ziliezuliwa na mvua hiyo na mapaa yake kutupwa mbali kabisa.
Alifafanua kuwa kaya tano za kijiji hicho hazina
mahali pa kuishi huku ng’ombe sita, mbuzi 34 zimekufa kutokana na mvua hiyo,
pamoja na bata, kuku 146 na magunia 72 ya mahindi vimesombwa na maji.
Mvua hiyo pia iliharibu migomba ekari moja na
mihogo ekari tatu ambayo haitegemei kuzalisha chochote tena.
Alisema kuwa hasara kamili haijajulikana na kwamba
bado wanaendelea kufanya tathmini ambapo taarifa za maafa hayo zimekwisha
kufikishwa kwa uongozi wa wilaya.
Chanzo: Tanzania Daima
0 comments:
Post a Comment