Home » » DC Tarime atupiwa kashfa nzito

DC Tarime atupiwa kashfa nzito



Mkuu wa Wilaya ya Tarime, John Henjewele
Hali siyo shwari katika wilaya ya Tarime, baada uongozi wa halmashauri ya wilaya hiyo kumtuhumu Mkuu wa Wilaya ya Tarime, John Henjewele kuunda asasi isiyo ya kiserikali kwa lengo la kuchota mamilioni ya fedha kutoka mgodi wa North Mara ambazo zimekuwa zikitolewa kwa ajili ya ufadhili wa masomo kwa wanafunzi wanatoka katika vijiji vinavyozunguka mgodi huo.
 Tuhuma hizo zimetolewa na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Tarime, Amos Sagara katika kikao kilichoitishwa na Katibu wa Itikani na Uenezi  wa CCM  Taifa, Nape Nnauye kwa  kusikiliza kero ambazo zimekuwa zikisabisha mahusiano mabaya kati ya wananchi na uongozi wa mgodi huo unaomilikiwa na kampuni ya African Barrick Gold.

 Katika kikao hicho kilichofanyika juzi katika mji mdogo wa Nyamongo na kuhudhuriwa na mkuu huyo wa wilaya, wakiwamo viongozi  wa vijiji vinavyozunguka mgodi huo na  wawakilishi wa wananchi, kiongozi huyo wa halmashauri ya Tarime alidai DC  Henjewele amekuwa chanzo kikuu cha kukosekana kwa amani katika eneo hilo.

 Alisema baada ya kuanzishwa mfuko wa elimu kwa ajili ya kusomesha wanafunzi wa vyuo mbalimbali wanaotoka katika vijiji vinavyozunguka eneo hilo, alidai kuwa mkuu huyo wa wilaya alizuia fedha hizo kuwekwa katika mfuko huo badala yake zinapelekwa ofisini kwake hatua ambayo imeshindwa kuwasaidia wananchi hao na hivyo kuzua mgogoro mkubwa.

 “Tatizo la hapa ni DC (mkuu wa wilaya) amekuwa akitumia fedha za mfuko wa elimu kama NGOs  yake kila kitu yeye  amekuwa  kinga kwa mgodi kushindwa kutekeleza mikataba…kila kitu ukiuliza unaambiwa muulize DC  hivi huyu mkuu wa wilaya ni nani katika mgodi wa North Mara?” alihoji Sagara huku akishangiliwa na viongozi wa vijiji na wawakilishi wa wananchi.

 “Kila tukidai  haki  za wananchi wetu ambazo zinaonekana kuporwa na mgodi, unakutana na vizingiti vingi eti unakuta DC anawajibia mgodi hauna  fedha …hii ni hatari sana bila kuchukua hatua dhidi ya mkuu wa wilaya  tatizo hili la mgogoro kamwe haliwezi kuisha” aliongeza.

Mkazi mmoja wa Nyamongo, Daud Makone alimtuhumu mkuu huyo wa wilaya kuchangia kuvuruga mahusiano mazuri yaliyokuwapo kati ya wananchi na uongozi wa mgodi huo.

“Miaka yote tumekuwa tukihamishwa bila vurugu wala watu kutishwa, tena tunapokea fidia na kuondoka …sasa tangu amekuja huyo mkuu wa wilaya imekuwa kero kubwa hatua ambayo imefanya kuwapo kwa uhasama mkubwa kati ya jamii na uongozi wa mgodi” alisema.

Hata hivyo, Mkuu huyo wa wilaya ya Tarime, Henjewele, alikanusha kuhusika na ubadhirifu wa fedha hizo za mfuko wa elimu, huku akisema hajawahi kuchukua fedha hizo kusomesha mtoto wake.

“Naomba mthibitishe hapa kama kweli kuna jina la mtoto wangu ambaye amewahi kusomeshwa na fedha za mgodi, tulifanya uchunguzi tukabaini kuwa fedha hizo  zimekuwa zikichakachuliwa na baadhi ya watumishi wa mgodi na tulipobaini tu tulichukua hatua ya kumwambia meneja wa mgodi na tayari watumishi wengine wamefukuzwa kazi” alisema na kuongeza.

 “Pia kuna baadhi ya watu wakiwamo viongozi  wa vijiji  wamekuwa wakiingiza majina hewa ambao si wahitaji wa kusomeshwa wa fedha hizo hatua ambayo ilisabisha mgodi kushindwa kuchangia fedha katika mfuko huu, sasa leo iweje mseme DC ndiye anahusika, mimi nafanya kazi kwa kufuata taratibu” alisema Henjewele.

Akizungumza katika kikao hicho, Nape Nnauye, alisema CCM haitakubali kuendelea kwa uhasama katika eneo hilo huku wananchi wakikosa haki zao kutokana na tamaa za baadhi ya viongozi.

“Nimesema nakwenda kukutana na Tamisemi ili watume watu wao kuja kuchunguza, tukibaini yoyote aliyehusika bila kujali pembe zake au ni nani tutamchukulia hatua kali zikiwamo za kisheria…hatuwezi kuendelea kwa mchezo huu” alisema Nape.

Wakati hatua hizo zikichukuliwa, amewaagiza viongozi wa vijiji waanze  mara moja mchakato wa kuanzisha mfuko mpya  na baada ya ngazi hiyo kukamilisha kazi hiyo ipelekwe kwenye  baraza la madiwani kwa ajili ya kupata baraka  zake ili uweze kuanza kazi.
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa