Home » » Mauaji ya kutisha Musoma

Mauaji ya kutisha Musoma

WATU watano wameuawa kikatili kwa kuchinjwa, kukatwa mapanga katika mfululizo wa matukio ya mauaji ya kinyama yanayoendelea kutokea katika wilaya  za Musoma, Butiama na Rorya mkoani Mara.
Kibaya zaidi, mauaji hayo ambayo yameendelea kutokea mfululizo ndani ya wiki moja, yamekuwa yakiwalenga zaidi wanawake wanapokuwa mashambani na wakati mwingine kuvamiwa majumbani mwao.
Mauaji ya kwanza yametokea hivi karibuni  katika Kijiji cha Mkirira, Kata ya Nyegina wilayani Butiama baada ya mwanamke mmoja kuuawa akiwa shambani kwake kisha wauaji kuchimba shimo fupi na kuufukia mwili wake.
Mauaji hayo yameibua hofu kubwa kwa wananchi hasa wanawake katika kijiji hicho kutokana na mfululizo wa mauaji ya aina hiyo ambapo hadi sasa wanawake wanne kati ya watu watano, wameuawa kwa kukatwa mapanga na kuchinjwa kama kuku.
Mauaji ya juzi ya mwanamke aliyejulikana kwa jina la Mkaguru Magee, yamesababisha wanawake  wa  kijiji  hicho kujifungia  ndani  na  kushindwa  kwenda  kwenye  shughuli  za kilimo kwa kuogopa kuuawa.
Siku moja baada ya mama huyo kuuawa kinyama, yakaibuka mauaji ya Mwenyekiti wa CCM Tawi la Nyakato kwa Sanane katika Manispaa ya Musoma mkoani Mara, Shaban Wambura aliyeuawa kwa kunyongwa kisha kutobolewa macho yote.
Baada ya mauaji hayo ya kikatili, wauaji walichukua mwili wa marehemu na kwenda kuutupa katika majaruba  ya mpunga maeneo ya Shule ya Msingi Mshikamano, mjini Musoma.
Baadhi  ya  watu wakiwemo watoto wa marehemu ambao walifika kushuhudia mwili  kabla ya kuchukuliwa na polisi, walisema kabla ya kifo chake mwenyekiti huyo alitoka nyumbani kwenda matembezini  ambako hakuweza kurudi hadi mwili wake ulivyokutwa  umetupwa katika eneo hilo.
Katika tukio jingine watu wasiojulikana wamewaua kikatili kwa kuwakata mapanga mama mmoja na kijana wake ambaye alikuwa amefaulu kujiunga na kidato cha kwanza katika Shule ya Sekondari Suba.
Mama na mwanaye huyo, walivamiwa na wauaji hao wakati wakipata chakula cha  usiku nyumbani kwao katika Kijiji cha Komuge wilayani Rorya mkoani Mara.
Mauaji  ya mama huyo,  Matinde Waryuba (46), yamefanyika saa mbili usiku katika kijiji hicho ambapo aliuawa kwa kuchinjwa na kukatwakatwa mapanga katika sehemu mbalimbali za mwili wake, huku mtoto wake wa mwisho, Thobias  Waryuba (14), naye akiuawa kwa kukatwa mapanga sehemu  za shingo na mabegani.
Ndugu wa marehemu, Prisca Misana, alisema hadi sasa familia haijatambua sababu za mauaji hayo ya kikatili huku wakitoa wito kwa serikali kuwasaka wauaji hao katika kuondoa hali ya kulipizana visasi.
Polisi mjini Musoma imethibitisha kutokea kwa mauaji hayo na kwamba hadi sasa uchunguzi  wa kina unafanywa kujua chanzo chake na kubaini wauaji ili waweze kufikishwa katika vyombo  vya sheria.
Kwa upande wao, baadhi ya wazee wa mila ambao wamekutana muda mfupi baada ya kutokea kwa mauaji hayo, wamelaani vikali vitendo hivyo vya kikatili, huku wakitaka serikali kupitia vyombo vya dola  kufanya uchunguzi wa kina kuhakikisha wauaji hao wanakamatwa na kufikishwa katika vyombo vya sheria.
Miili ya  marehemu hao imechukuliwa na polisi wa Wilaya ya Rorya kwa uchunguzi zaidi na kisha kuhifadhiwa katika chumba cha  maiti cha hospitali ya serikali ya Mkoa wa Mara mjini Musoma na inatarajia kuzikwa kesho.
Wakizungumza baada wajumbe wa Kamati  ya  Ulinzi na Usalama wakiongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Butiama, Angelina Mabula,  wananchi  wa kijiji hicho  wameitaka  serikali  kuchukua  hatua  za  haraka kumaliza  mauaji  hayo, kwani   hivi  sasa  hakuna mwanamke  anayekwenda shambani  bila  ya  ulinzi.
“Shughuli za kilimo zimesimama, wanawake wote wameogopa kwenda shambani, mfano mimi ndio mtafutaji, lakini leo mke wangu ameniambia nimpeleke shamba kutokana na hofu hiyo, sasa tutaishi vipi?” alihoji Jumanne Magafu.
Kwa upande wake, mkazi mmoja ya kijiji hicho, Maria Majura, aliiomba serikali licha ya kufanya doria za usiku, pia polisi wahusike kufanya doria za mchana ili kukabiliana na mauaji hayo ya kikatili.
Kwa upande  wao,  viongozi  wa Chama  Cha Mapinduzi (CCM)  ngazi  ya  mkoa  na taifa, wakiongozwa na Katibu wa UWT Taifa, Amin Makiragi, wamelaani   mauaji  hayo ya  kikatili  huku  wakitaka  vyombo  vya  dola  kuwasaka  wauaji  hao na kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria.
Mkuu  wa Operesheni  wa Jeshi la Polisi  Mkoa wa Mara, Oudax Majaliwa, ameomba jamii  kutoa  ushirikiano kwa  vyombo  vya  ulinzi  na  usalama  kufanikisha  kukamatwa  kwa  wauaji  hao.

Mtoto na mjukuu wa Meja Jenerali Marwa wauawa
Wakati huo huo, Mwandishi Igenga Mtatiro anaripoti kuwa aliyekuwa askari wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ)  na aliyehitimu mafunzo ya ukomandoo wa jeshi hilo, Zacharia Chacha Marwa ambaye ni mtoto wa Marehemu Meja Jenerali, Mwita Marwa, ameuawa kwa kupigwa risasi usiku wa kuamkia jana.
Mwingine aliyeuawa katika tukio hilo ni mjukuu wa Meja Jenerali Marwa, Erick Lucas Mohabe (24) ambaye pia aliuawa kwa kushambuliwa na risasi katika tukio hilo hilo.
Mauaji hayo yalitokea katika Kijiji cha Mogabiri, Kata ya Ketare, Tarafa ya Inchage, Wilaya ya Tarime mkoani  Mara.
Kwa mjibu wa mdogo wa marehemu, aliyejulikana kwa jina la Joseph Marwa, waliouawa ni ndugu zake na hadi sasa hawajui chanzo cha mauaji yao.
Kamanda wa Polisi Tarime na Rorya, Justus Kamugisha, alithibitisha kutokea tukio hilo na kwamba askari walikuwa wanaendesha msako mkali kuwabaini wahusika hao.
Chanzo;Tanzania Daima 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa