Home » » UPUNGUFU WA WAALIMU TATIZO BUNDA

UPUNGUFU WA WAALIMU TATIZO BUNDA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
IDARA ya Elimu katika Wilaya ya Bunda mkoani Mara, inakabiliwa na changamoto  mbalimbali ikiwamo upungufu wa walimu, migogoro ya mipaka ya maeneo ya shule, utoro wa wanafunzi na kitengo cha ukaguzi kukosa chombo cha usafiri.
Hayo yalibainishwa jana katika mkutano wa kuboresha elimu wilayani hapa, uliofanyika katika Ukumbi wa Chuo cha Ualimu Bunda, mjini hapa.
Ofisa Elimu wa Shule za Msingi wilayani hapa, Jeshi Lupembe, alisema kuna upungufu wa walimu 236 na kwamba katika mgawo wa walimu wapya, wamefanikiwa kupata walimu 86, huku wanaostaafu mwaka huu wakiwa 65.
Lupembe alisema changamoto nyingine ni mwamko duni wa wazazi na walezi kuchangamkia elimu, kwani baadhi yao hawafuatilii mienendo ya masomo ya watoto wao.
Changamoto nyingine aliitaja kuwa ni ukosefu wa usafiri kwa ajili ya ukaguzi, kwa sababu gari lililopo ni bovu, kutokuwepo usimamizi wa mara kwa mara na ukosefu wa chakula cha wanafunzi kwa baadhi ya shule.
Ofisa Elimu wa Shule za Sekondari wilayani hapa, Martin Nkwabi, alisema changamoto kubwa ni upungufu wa walimu wa masomo ya sayansi, hali ambayo imekuwa ikisababisha wanafunzi kutokufanya vizuri katika masomo hayo.
Nkwabi alisema pamoja na kuwa na upungufu wa walimu wa masomo ya sayansi 158, lakini katika mgawo wa walimu wapya wamefanikiwa kupata walimu 15 wa somo hilo, na kwamba hadi sasa walioripoti ni wanane.
Alisema changamoto nyingine ni upungufu wa vifaa vya kufundishia na kujifunzia, ikiwa ni pamoja na vitabu vya maabara na dawa na nyenzo nyinginezo.
Naibu Mkaguzi Mkuu wa Shule za Msingi wilayani hapa, Anna Ouma, alisema kitengo hicho kinakabiliwa na changamoto nyingi, ambazo inatakiwa zipatiwe ufumbuzi haraka ili kuinua kiwango cha elimu.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa