Home » » NERUMA BUNDA WAWATOSA WAKOPESHAJI BINAFSI

NERUMA BUNDA WAWATOSA WAKOPESHAJI BINAFSI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

KUTOKANA na kuibuka kwa wakopeshaji binafsi wanaotoza riba kubwa kwa watu wanaokopeshwa fedha, wakulima, wafanyabiashara na watumishi wa serikali Kata ya Neruma, Wilaya ya Bunda, mkoani Mara, wameamua kuanzisha Chama cha Kuweka Akiba na Kukopa, ili waweze kuondokana na kero hiyo ya kunyonywa.
Chama hicho chenye makao yake makuu Kijiji cha Kasahunga wilayani hapa, kinajulikana kwa jina la Neruma Initiative Social Development Association (Nisa), ambacho kwa sasa kina mtaji wa zaidi ya sh milioni 40.
 Aidha, ushirika huo una wanachama 37, ambao ni wakulima, wafugaji, wafuvi na wafanyakazi wa serikali kutoka katika sekta ya elimu na afya, waliyoko kijiji cha Kasahunga.
Akitoa taarifa kwenye mkutano mkuu wa mwaka wa chama hicho, Mwenyekiti wa ushirika huo, Josephat Malima, alisema waliamua kuuanzisha kutokana na kero hiyo ya kukopeshwa kwa riba kubwa na wakopeshaji hao binafsi.
Malima, alisema kuwa wakopeshaji hao wamekuwa wakiwakata riba ya zaidi ya asilimia 50 hadi 60 na kwamba huo ni unyonyaji mkubwa.
“Sisi watumishi wa serikali, pamoja na wakulima na wavuvi tuliamua kuanzisha ushirika huu, ili tuweze kuondokana na kero ya kukopa kwa watu binafisi ambao hutoza riba kati ya asilimia 50 hadi 60, sasa sisi tunakupoeshana kwa riba ndogo tu ya asilimia tano,” alisema.
Alisema kuwa tangu walipoanzisha chama hicho Julai 3, 2012, wanachama wake wamekwishapata mfanikio makubwa, ikiwa ni pamoja na kuchukuwa mikopo ya masharti nafuu na kuitumia kwa kusomesha watoto wao, kuanzisha maduka na kununua pikipiki kwa ajili ya kufanyia biashara ya kubeba abiria (bodaboda).
Awali Katibu wa chama hicho, Charles Tizirukwa, alisema lengo lao jingine ni kutaka kusaidia watoto wanaoishi katika mazingira hatarishi zaidi, kwa kuwapatia mahitaji ya kibinadamu, ikiwemo elimu, sanjari na kutoa mikopo ya masharti nafuu kwa wananchi wengine wa nje na ushirika huo.
Kwa upande wake, mgeni rasmi katika mkutano huo ambaye alikuwa Ofisa Tarafa ya Kenkombyo, Peter Jandwa, aliyemwakilisha Mkurugenzi wa shirika la Zinduka, linalosaidia watoto wanaoishi katika mazingira magumu, Maxi Madoro, aliwataka wananchi wengine kuiga mfano huo, kwa kuanzisha vyama vya kuweka akiba na kukopa ili waweze kujiinua kiuchumi na kuondokana na umasikini
 Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa