Home » » WALIMU WALIA UHABA WA NYUMBA BUNDA

WALIMU WALIA UHABA WA NYUMBA BUNDA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 
WALIMU wa shule ya Msingi Nafuba, iliyoko katika kisiwa ndani ya Ziwa Victoria, Wilaya ya Bunda mkoani Mara, wanafanya kazi katika mazingira magumu, ikiwa ni pamoja na familia mbili kuishi nyumba moja yenye vyumba viwili.
Hali hiyo, imebainika juzi baada ya Ofisa Elimu shule za Msingi Bunda, Jeshi Pembe, kutembelea shule hiyo na kujionea hali halisi ya mazingira na jinsi walimu wanavyofanya kazi katika mazingira magumu.
Wakitoa kero yao kwa Ofisa Elimu huyo, walimu hao wakiongozwa na Mwalimu Mkuu, Gatawa Magaji, walisema shule hiyo ina upungufu mkubwa wa nyumba za walimu, kwani kwa sasa ziko mbili tu.
Walisema kuwa, katika nyumba moja yenye vyumba viwili bila dari, zinaishi familia mbili za walimu, akiwemo mwalimu mkuu na kwamba, jambo hilo ni aibu kubwa, hasa ukizingatia juu iko wazi.
Waliongeza kuwa, kutokana na hali hiyo ya ufinyu wa nyumba hiyo na aibu kwa familia zao, wamelazimika kupangisha vyumba vingine uraiani ili watoto wao ambao ni wakubwa, waweze kulala huko.
“Aibu hii unayoiona inatufanya tupange vyumba vingine kwenye miji ya wananchi, ili watoto wetu wakubwa waweze kulala huko….yaani kwa ujumla sisi huku tunafanya kazi katika mazingira magumu,” alisema mwalimu Mbita Maagi.
Walibainisha kutokana na kutokuwepo nyumba za kutosha, ndio maana walimu wengi wamekuwa hawataki kufundisha kwenye shule hiyo iliyoko kisiwani.
Walisema kuwa, kwa sasa wapo walimu watano tu wanaofundisha wanafunzi 570 wa darasa la kwanza hadi la saba, ambako kila mwalimu hufundisha watoto zaidi ya 100, ambako ikama mwalimu mmoja anatakiwa kufundisha wanafunzi 45 tu.
Kutokana na changamoto hizo, Ofisa Elimu huyo aliyehamia wilayani hapa hivi karibuni, pamoja na kusikitishwa na hali hiyo, alisema katika mipango yake ya kuinua elimu Bunda, atachukuwa hatua zaidi kwa kuipatia kipaumbele shule hiyo, ili iweze kupata nyumba za walimu pamoja na kuongeza walimu zaidi.
Pembe, alisema haipendezi kabisa familia za walimu wawili kuishi kwenye nyumba moja, tena isiyokuwa na dari kwa sababu hiyo ni aibu kubwa.
Katika hatua nyingine, walimu wa shule hiyo walimpongeza Ofisa Elimu huyo kwa kuwatembelea na kuona mazingira wanayofanyia kazi, pamoja na kushuhudia changamoto zinazowakabili, ambako pia wamewataka viongozi wengine kuiga mfano huo.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa