Home » » WANANCHI WALALAMIKIA MATUMIZI MABAYA YA FEDHA

WANANCHI WALALAMIKIA MATUMIZI MABAYA YA FEDHA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 
WANANCHI wilayani Bunda, mkoani Mara, wamelalamikia kitendo cha madiwani wa wilaya hiyo, kutumia fedha na kuunda tume ya watu watatu, akiwemo mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Joseph Malimbe, kwenda kumuona Katibu Mkuu kwa ajili ya kusitisha uhamisho wa mganga mkuu wa wilaya hiyo.
Wakizungumza katika kikao cha Baraza la Madiwani, wananchi hao walisema kuwa ni matumizi mabaya ya fedha za wananchi kwa viongozi hao kuamua kwenda mkoani Dodoma kwa ajili ya kusitisha uhamisho wa mtumishi huyo ambao ulikuwa ni halali kwa mujibu wa sheria.
Walisema kuwa wameshangazwa na kitendo hicho kilichofanywa na viongozi hao kuamua kuunda tume hiyo wakati uhamisho huo umefanyika kwa mujibu wa sheria.
Mmoja wa wananchi hao, Ascetic Malagila walisema kuwa baraza hilo limetumika vibaya fedha za wananchi ambapo inasemekana wametumia zaidi ya sh milioni sita kwa ajili ya safari hiyo.
“Mganga mkuu Charle Nkombe, aliletewa barua ya uhamisho kutoka Tamisemi lakini baada ya kupata taarifa hiyo, baraza la madiwani likiongozwa na mwenyekiti huyo waliupinga na kuunda tume ili waweze kumuona Katibu Mkuu ili afute uhamisho huo,” alisema.
Alisema kuwa amelazimika kuandika kulalamikia matumizi mabaya ya fedha hizo ambapo nakala ya barua hiyo ameituma Katibu Mkuu wa Tamisemi, Afisa Usalama wa taifa wa wilaya hiyo, Mkuu wa Wilaya, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Mbunge wa jimbo la Bunda na Mwibara, pamoja na madiwani wote wa Halmashauri hiyo.
Malagila alisema kuwa kisheria mwajiri anayo haki ya kumpa uhamisho mtumishi yoyote na kumpeleka popote pale nchini.
Alisema kuwa fedha hizo zimetumika vibaya kwani ni vema zingeelekezwa katika shughuli za maendeleo hususani, ununuzi wa madawati ili kuwaepusha watoto kukaa chini.
Akizungumza na Tanzania daima kujibu malalamiko hayo, Mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Malimbe, alisema kuwa hilo ni azimio la baraza la madiwani na kwamba wananchi hawapo juu ya baraza hilo na wala hawapaswi kuhoji maamuzi hayo.
“Kwa hiyo wewe na hao wananchi mnapinga maamuzi ya Baraza la madiwani” alisema na kukata simu na kisha akatuma ujumbe wa simu ya mkononi akisema, “Mheshimiwa Makongo, kila chombo kina taratibu za kujiendesha. Siku ya baraza ulikuwepo unajua maamuzi ya baraza ndicho chombo cha maamuzi ya mwisho”
Chanzo:Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Mara Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa